http://www.mkcomputertweaks.com/mkgroup/fkbmksb.gifMatangazo

Tangaza nasi: mkatedaniel@gmail.com, +255 7666-00 69 70, +255 655-00 69 71, +255 787- 249594

Usilikose kila Jumapili

Jumatano, 22 Mei 2013

CRDB YATOA VIFAA VYA MICHEZO KWA WANAJESHI WANAOENDA DRC


ILI kuwapa hamasa Wanajeshi wa Jeshi la Ulinzi wa Tanzania (JWTZ) wanaoenda kulinda amani Jamhuri ya Kidemokrasia ya kondo (DRC), benki ya CRDB imetoa msaada wa vifaa vya michezo kwa askari hao vikiwa na thamani ya Sh.milioni 6.8.
Msaada huo ulitolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Dk. Charles Kimei kwa niaba ya benki yake, na kumkabidhi Mnadhimu Mkuu wa JWTZ, Luteni Jenerali Samweli Ndomba, aliyepokea kwa niaba ya mkuu wa majeshi nchini.
Akizungumza katika makabidhiano hayo, Dk Kimei alisema vifaa hivyo vya michezo vinatolewa kwa ajili ya wanajeshi wanaoenda kulinda amani DRC ili kuweza kuburudika katika michezo wakati wa mapumziko.
“CRDB inajua nyie ni wateja wetu wazuri, hivyo tumeamua kutoa msaada huu kwa wanajeshi wanaoenda kujilinda amani ili kuweza kuwapa hamasa vijana wetu watakapokuwepo huko,” alisema Dk. Kimei.
Vifaa hivyo vilivyotolewa na benki hiyo ni jezi za soka, netiboli, khanga na vitenge kwa ajili ya wanajeshi wa wanawake watakaokuwa wakicheza ngoma wakati wa mapumziko.
Akipokea msaada huo, Luteni Jenerali Ndomba alianza kwa kuishukuru benki hiyo kwa kutoa vifaa hivyo wakati wanajeshi wakijiandaa na safari ya kuelekea DRC.
“Si mara yenu ya kwanza kutoa vifaa kama hivi, hata wakati ule vijana wetu walipokuwa wakilinda amani Darfur, mlitupa msaada kama huu…tunashukuru sana kwa hilo, na pia msaidie hata kutoa vifaa kwa timu za majeshi za hapa nyumbani ” alisema Luteni Jenerali Ndomba.
Aidha, Ndomba aliishukuru benki hiyo kwa kuweza kuahidi kutoa mikopo ya riba nafuu ya nyumba kwa wanajeshi wa jeshi lake.